Headlines News :
Home » » MKUTANO MKUU SIMBA SC KUFANYIKA JULAI 20

MKUTANO MKUU SIMBA SC KUFANYIKA JULAI 20

Written By Bashir Nkoromo on Sunday, July 7, 2013 | 11:51 PM


KLABU ya Simba imepanga kufanya mkutano wake mkuu wa mwaka wa wanachama Julai 20 mwaka huu.

Kaimu Makamu Mwenyekiti wa Simba, Joseph Itang'are alisema jana kuwa, mkutano huo utafanyika kwenye Bwalo la Maofisa wa Polisi, Oysterbay, Dar es Salaam.

Itang'are, maarufu kwa jina la Kinesi alisema, uamuzi wa kuitisha mkutano huo taehe hiyo, ulifikiwa katika kikao cha kamati ya utendaji kilichofanyika juzi na jana mjini Dar es Salaam.

Alizitaja ajenda zitakazojadiliwa katika mkutano huo kuwa ni pamoja na kupokea taarifa mbalimbali za msingi za klabu kwa mwaka mzima, ikiwemo ripoti ya mapato na matumizi kwa mwaka mzima.

Ajenda zingine ni ushiriki wa Simba katika michuano ya ligi kuu ya Tanzania Bara msimu uliopita pamoja na ombi la kujiuzulu kwa aliyekuwa makamu mwenyekiti wa klabu hiyo, Geofrey Nyange 'Kaburu'.

Kinesi alisema tayari maandalizi kwa ajili ya mkutano huo yameshaanza na amewataka wanachama kujitokeza kwa wingi kuhudhuria ili waweza kujadili mambo mbalimbali yanayoihusu klabu yao.

Kuitishwa kwa mkutano huo kumekuja siku chache baada ya baadhi ya wanachama kuushinikiza uongozi chini ya Mwenyekiti, Ismail Aden Rage uitishe mkutano kwa ajili ya kujadili kuvurunda kwa Simba katika ligi.

Wakati huo huo, kamati ya utendaji ya Simba imeridhia kuongezwa mikataba kwa Kocha Msaidizi wa timu hiyo, Jamhuri Kihwelo 'Julio' na Ofisa Habari wa klabu, Ezekiel Kamwaga.

Katika kikao hicho, wajumbe pia waliridhia kiungo wa timu hiyo, Kigi Makasi apelekwe India kwa ajili ya kupatiwa matibabu ya goti baada ya kuumia wakati wa mechi ya kirafiki kati ya Simba na CDA iliyochezwa mjini Dodoma.

Katika hatua nyingine, klabu ya Simba inatarajia kufanya ziara katika vituo mbalimbali vya watoto yatima na kutembelea wagonjwa kuanzia Agosti 5 hadi 11 mwaka huu.

Ziara hiyo ni miongoni mwa shughuli mbalimbali za kijamii, ambazo Simba itazifanya katika wiki ya kuelekea Tamasha la Simba, maarufu kwa jina la 'Simba Dar'.

Katika wiki hiyo, wachezaji na viongozi wa Simba pia watahudhuria kozi maalumu, itakayoandaliwa na wadhamini wa klabu hiyo, Kampuni ya Bia Tanzania (TBL) na kutembelea shule za msingi kwa lengo la kuwahamasisha watoto wapende mchezo wa soka.

Shughuli zingine zitakazofanywa na Simba katika wiki hiyo ni pamoja na kutembelea vyombo vya habari na kusoma hitma kwa ajili ya kuwarehemu wachezaji, viongozi na wanachama wa klabu hiyo waliotangulia mbele ya haki
Share this article :

0 comments:

Speak up your mind

Tell us what you're thinking... !

Total Pageviews

Comments

 
Support : Creating Website | Johny Template | Mas Template
Proudly powered by Blogger
Copyright © 2011. theNkoromo SPORTS - All Rights Reserved
Template Design by Creating Website Published by Mas Template